Katika barua rasmi ya kujiuzulu iliyowasilishwa kwa Rais wa Jamhuri, Mutamba amesema:
“Ninachagua kujiuzulu kwa hiari yangu mwenyewe, mbele ya taifa, ili nisije nikageuka kikwazo kwa kazi ya serikali na kuhifadhi heshima ya taasisi ya haki ninayotumikia.”
Mutamba, ambaye hadi wakati wa kujiuzulu kwake alikuwa Waziri wa Haki na Kiongozi wa Harakati ya Mapinduzi ya Kidemokrasia ya Kizalendo (MRDP), amekuwa kwenye vichwa vya habari katika wiki za hivi karibuni kutokana na mashitaka yanayomkabili kuhusu matumizi mabaya ya fedha za umma, hasa dola milioni 39 zilizotengwa kwa ujenzi wa gereza la Kisangani.
Wakati baadhi ya wachambuzi wa siasa wakiona kujiuzulu kwake kama ishara ya uzito wa kesi dhidi yake, wafuasi wake wanaona kuwa ni hatua ya kisiasa inayolenga kumdhalilisha. Mutamba mwenyewe amepinga vikali mashitaka hayo, akisema ni njama ya kisiasa iliyoandaliwa ili kumzuia kupigania haki na mabadiliko ya kweli katika mfumo wa sheria wa nchi hiyo.
Kujiuzulu kwa Mutamba kunakuja siku chache baada ya Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Rufaa, Firmin Mvonde, kuagiza asizuiliwe kuondoka Kinshasa, akihofia kwamba angeweza kukimbia kabla ya hatua za kisheria kukamilika.
Kwa sasa, bado haijafahamika wazi ikiwa Rais Tshisekedi atakubali mara moja kujiuzulu kwa Mutamba au kama kutakuwa na mashauriano zaidi ndani ya serikali na bunge. Hata hivyo, tukio hili linazidi kuibua maswali kuhusu mustakabali wa vita dhidi ya ufisadi nchini, na jinsi gani serikali inaweza kutenganisha kati ya uwajibikaji wa kweli na maamuzi ya kisiasa.
Kwa Muhtasari:
- Constant Mutamba ametangaza kujiuzulu kwa Rais Tshisekedi.
- Anakabiliwa na mashitaka ya ufisadi wa mamilioni ya dola.
- Anadai anaandamwa kisiasa.
- Hatua yake imezua maoni mseto kuhusu hali ya kisiasa na sheria nchini RDC.