“Mambo mengi hayaendi vizuri. Nimekwisha kuwasilisha ripoti kadhaa kwa Rais wa Jamhuri, hata kabla ya kuanguka kwa mji wa Goma. Baadhi ya vikosi vilikuwa na askari 300 pekee badala ya 1,500 waliotarajiwa. Hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa. Tatizo la idadi ya wanajeshi bado halijapatiwa suluhisho,” alisema kwa uchungu.
Wajane wa mashujaa wa taifa wakisahaulika
Kwa Jenerali Luboya, hali imezidi kuwa mbaya sasa kwa sababu wake wa wanajeshi waliouawa vitani hawapokei tena mafao yao, licha ya mchango mkubwa walioutoa wa kuwakilisha taifa vitani kwa niaba ya familia zao.
“Kinachoumiza zaidi ni kwamba hali hii inatokea katika eneo la operesheni, ambako vita vinaendelea. Unatarajia vipi mwanajeshi anayepambana mstari wa mbele awe na moyo wa kupigana, wakati anasikia kwamba mjane wa mwenzake aliyeuawa hatimiziwi haki yake ya msingi? Atajiuliza: ‘Nikifa, familia yangu nao watatelekezwa hivi hivi?’” alisema kwa masikitiko.
Kauli hii ya Gavana Luboya inakuja wakati ambao jeshi la FARDC linaendelea na mapambano magumu dhidi ya makundi yenye silaha kama ADF, CODECO na mengineyo katika maeneo ya Ituri, Kivu Kaskazini na Haut-Uélé. Lakini motisha ya askari, hasa wale walioko mstari wa mbele, inapungua kwa kasi, kutokana na kuona kwamba hata waliotoa uhai wao kwa ajili ya taifa hawaheshimiwi baada ya kufa.
Wito kwa mamlaka ya juu kuchukua hatua
Jenerali Luboya ametaka serikali kuu, hususan Ikulu ya Rais, ichukue hatua za haraka na za wazi kuhakikisha mafao ya wajane wa mashujaa wa taifa yanarejeshwa na kulipwa kwa wakati. Ameonya kuwa hali hii inaweza kuzidisha mmomonyoko wa maadili ndani ya jeshi na kuathiri kwa kiasi kikubwa morali wa wanajeshi walio kazini.
Kauli ya Jenerali Luboya ni kilio cha uongozi wa mstari wa mbele, unaotaka kuona haki za msingi za familia za mashujaa wa taifa zikizingatiwa. Katika wakati huu ambapo nchi inahitaji mshikamano na ari ya kulinda taifa, kusahau wajane wa wanajeshi waliokufa vitani ni kosa lisilovumilika – la kiutu na la kimaadili.