Katika hotuba aliyotoa mbele ya wakazi wa Bunia, mji mkuu wa Ituri, Jenerali Luboya alisema: “Kama mkiona mashine zangu katika migodi ya dhahabu mahali popote hapa Ituri, zichomeni moto. Mimi ni mwanajeshi, kazi yangu ni kuwarudishia amani, si kuchimba dhahabu.”
Kauli hiyo imekuja wakati ambapo wasiwasi unaendelea kuongezeka juu ya ushiriki wa baadhi ya maofisa wa kijeshi katika biashara haramu ya madini, ambayo inachochea vita na mateso kwa raia wa kawaida.
Luteni Jenerali Luboya, anayeheshimika kwa msimamo wake wa kutetea usalama wa raia, ameweka wazi kuwa haruhusu askari au viongozi kutumia nafasi zao kujinufaisha na utajiri wa nchi wakati wananchi wanateseka.
Amesisitiza kuwa jukumu lake kuu ni kuimarisha usalama, kupambana na makundi ya waasi, na kuhakikisha wakazi wa Ituri wanaishi kwa amani bila hofu ya mashambulizi au uporaji wa mali yao.
Wakazi wengi wa Bunia wamempongeza kwa ujasiri wake na kauli hiyo ya wazi, wakisema ni matumaini mapya ya kuona mabadiliko ya kweli katika uongozi wa kijeshi nchini.