Kikaya, aliyekuwa balozi wa Kongo nchini Uingereza na mshauri wa kidiplomasia wa Kabila kwa muda mrefu, alipewa jukumu la kufanya mawasiliano ya “kijamii na kisiasa” na baadhi ya wadau wa kimataifa mjini Washington. Hata hivyo, ujumbe alioutoa mbele ya vyombo vya habari ulifichua hali ya wasiwasi mkubwa ndani ya kambi ya Kabila kuhusu mwelekeo wa nchi.
“RDC iko katika hali ya hatari ya kupasuka kutoka ndani. Kukimbilia makubaliano na Rwanda, bila kushughulikia chanzo halisi cha mzozo – ambacho ni uvamizi, uporaji wa maliasili, na udhaifu wa taasisi zetu ni sawa na kujidanganya. Historia haitusamehi kwa hilo,” alisema Kikaya kwa msisitizo.
Kwa nini Kabila anakaa kimya kuhusu Rwanda?
Hili ndilo swali ambalo linaendelea kuwagawanya wachambuzi wa siasa za Kongo. Wakati viongozi wa sasa wa serikali ya Félix Tshisekedi wakitoa matamko ya moja kwa moja dhidi ya Rwanda, Kabila amebaki kimya. Kikaya alijibu swali hili kwa umakini mkubwa:
“Joseph Kabila ni mtu wa vuguvugu la kimkakati. Anaamini katika mazungumzo ya ndani kwa ndani na sio kulaani hadharani. Ameishi changamoto za uongozi kwa miaka zaidi ya kumi, na anafahamu kuwa matatizo ya Kongo hayawezi kutatuliwa kwa kejeli au maneno makali,” alisema.
Lakini wachambuzi wengine wanaona kuwa ukimya huu wa Kabila huenda unahusiana na historia yake ya ushirikiano wa kisiasa na kijeshi na Rwanda katika kipindi chake cha uongozi, hasa mwanzoni mwa miaka ya 2000, wakati alipofikia makubaliano kadhaa ya usalama na Paul Kagame.
Msimamo wa Kabila kuhusu M23: Halisi au wa kisiasa?
Kwa mujibu wa Kikaya, Kabila hana uhusiano na waasi wa M23 na wala haungi mkono harakati zao. “Wale wanaodai kwamba yeye ni sehemu ya njama hiyo wanapotosha. Msimamo wake uko wazi: Kongo ni moja, haiwezi kugawanywa wala kudhibitiwa kwa kutumia silaha,” aliongeza.
Hata hivyo, wachunguzi wa kisiasa wanahoji kama ukimya huo ni ishara ya kupendelea upande mmoja au ni mkakati wa kujitenga na hali ya kisiasa ya sasa ili kulinda turathi yake ya kisiasa.
Diplomasia ya kivuli au maandalizi ya kurejea?
Wengine wanaona safari ya Kikaya Washington si tu kwa ajili ya “mawasiliano”, bali ni dalili ya harakati za Kabila kujiandaa kwa muktadha mpya wa kisiasa nchini, hasa wakati ambapo wananchi wengi wanazidi kutoridhishwa na namna serikali ya sasa inavyokabiliana na uasi mashariki mwa nchi.
Kwa sasa, bado haijulikani iwapo Kabila atarudi tena kwenye ulingo wa kisiasa au ataendelea kuwa mtazamaji kimya wa mambo. Lakini kupitia ujumbe wa Kikaya, ujumbe umetumwa ukimya wake haupaswi kuchukuliwa kuwa udhaifu, bali ni sehemu ya mkakati.
Kauli za Kikaya bin Karubi zimefufua upya mjadala kuhusu nafasi ya Rwanda katika mgogoro wa Kivu, uhusiano wake na M23, na kwa kiasi kikubwa, nafasi ya Joseph Kabila katika siasa za sasa na za baadaye za DRC. Katika kipindi hiki kigumu, kila neno lina uzito na kila ukimya, tafsiri.